Bukobawadau

BUNGE LA BAJETI WABUNGE WAPANGUA KANUNI

Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe akiuliza swali katika kikao cha kwanza cha Mkutano wa 11 wa Bunge la Bajeti, Dodoma Picha na Edwin Mjwahuzi
 Spika wa Bunge, Anne Makinda akipitia makabrasha yake wakati akiongoza kikao cha kwanza cha Mkutano wa 11 wa Bunge la Bajeti, Dodoma jana

Dodoma. Baada ya siku mbili za mjadala mzito kuhusu mabadiliko ya Kanuni za Bunge, jana Bunge limepitisha azimio la mabadiliko yanayohusu utaratibu wa kutunga sheria kuhusu mambo ya fedha pekee.

Kwa uamuzi huo, mambo mengine ambayo yalikuwa yamependekezwa lakini hayahusiani na sehemu hiyo, yaliachwa baada ya kuibua mjadala mzito na kupingwa na baadhi ya wabunge.
Miongoni mwa mabadiliko yaliyofanyika, muda wa kuchangia hoja kwa wabunge katika Mkutano wa Bajeti unaoendelea umepunguzwa kutoka dakika 15 hadi 10, huku wabunge wakipigwa marufuku kutumia muda wao adhimu kutoa pongezi na pole, bali kuingia moja kwa moja kwenye hoja.

Hayo yaliamualiwa jana bungeni baada ya Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni za Bunge na Naibu Spika, Job Ndugai kuwasilisha azimio la marekebisho ya kanuni za Bunge ambalo lilipitishwa.

Akichangia hoja ya azimio hilo Mnadhimu Mkuu wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Tundu Lissu hakutaka muda wa kuzungumza upunguzwe kwa kuwa sehemu hiyo ni sehemu ya mazungumzo na si vinginevyo.

Hata hivyo Lissu ambaye pia ni Mbunge wa Singida Mashariki alikubaliana na pendekezo la kubadili muda kutoka dakika 15 hadi 10 akieleza kuwa litatoa nafasi kwa wabunge wengi kuchangia.

Mbunge wa Viti Maalumu (CCM), Anna Abdallah alisema mabadiliko hayo yanalipa Bunge uwezo wa kuisimamia Serikali katika mambo ya fedha.Mbunge wa Wawi, Hamad Rashid alisema dakika 10 ni nyingi na mtu akijipanga vizuri zinatosha kukamilisha hoja zake.

Suala jingine ambalo limefanyiwa mabadiliko ni kuwekwa uwiano wa kuchangia hoja ambapo wabunge sasa watapangwa kulingana na idadi yao kivyama.
Next Post Previous Post
Bukobawadau